Waziri, mkuu wa majeshi wavutana kuhusu ukuta Mererani kulindwa na Wanyarwanda

Na Mwandishi Wetu

 

BADO wakubwa wamegawanyika na wametikisika kuhusu sakata la ukuta wa Mererani, unaozunguka machimbo ya madini ya Tanzanite mkoani Manyara, kulindwa na wanajeshi kutoka Rwanda, SAUTI KUBWA linaeleza kwa uhakika.

 

Licha ya ukweli kuwa kuna wanajeshi wanakerwa na suala hilo, wapo wengine wasioona tatizo, na wanasiasa wameingilia kati kumkingia kifua Rais John Magufuli ambaye ndiye aliamua “kuajiri wanajeshi wa Rwanda” katika mradi huo.

 

Hata wiki iliyopita, baada ya SAUTI KUBWA kuibua sakata hilo,  kwamba limesababisha minong’ono miongoni mwa vyombo vya ulinzi, mkuu wa majeshi aliomba kifanyike kikao cha dharura kati yake na waziri wa ulinzi ili “kupata mwafaka na kuondoa nchi katika aibu hii.”

 

Mapema wiki inayomalizika leo, Dk. Hussein Mwinyi, ambaye ni waziri mwenye dhamana, na Jenerali Venance Mabeyo, mkuu wa majeshi,  walifanya kikao katika hoteli moja maarufu ufukweni mwa Bahari ya Hindi, eneo la Masaki. Kwa sababu maalumu, SAUTI KUBWA inahifadhi jina la hoteli hiyo.

 

Kilikuwa kikao cha watu watatu – Dk. Mwinyi, Mabeyo, na Dotto Biteko, naibu waziri wa madini. Wote watatu walielezana jinsi walivyoshangazwa na kuvuja kwa taarifa za ulinzi wa mradi huo, na walitafakari athari zake kwa heshima ya jeshi na taifa, na jinsi ya kuepusha madhara yatokanayo na uvujaji huo. Wazungumzaji wakuu katika kikao hicho walikuwa Dk. Mwinyi na Jenerali Mabeyo. Kila mmoja alikuwa na pendekezo lililopingwa na mwenzake.

 

Kwa mujibu wa vyanzo vyetu, kabla na baada ya uvujaji wa habari hizo, Jenerali Mabeyo amekuwa anakerwa na jinsimradi huo unavyosimamiwa, na msimamo wake unawakilisha msimamo wa wanajeshi wengi wanaoona kwamba “jeshi letu limedharauliwa.”

 

Katika kikao hiki, Jenerali Mabeyo alipendekeza kwamba kwa kuwa suala hili limeshavuja, ingekuwa vema serikali ichukue hatua ya haraka kurekebisha hali hiyo ili kudhibiti chokochoko na maneno ambayo yameanza kutoka.

 

“Pendekezo la mkuu wa majeshi ni kwamba rais ashauriwe, Wanyarwanda walio Mererani waondolewe, badala yake wapelekwe wanajeshi wa Tanzania kulinda ukuta,” kinasema chanzo hicho, na kuongeza kuwa hata hivyo, waziri hakukubaliana naye.

 

Kinaongeza: “Waziri ana msimamo tofauti. Yeye anasisitiza kwamba rais aachwe afanye atakavyo, asilazimishwe kufuata maneno ya watu.” Chanzo hicho kinamkunuu waziri akisema: “tusifuate maneno ya watu kubadili msimamo wa rais. Wanajeshi (wanyarwanda) waachwe wafanye wanaloliamini kama walivyoagizwa.”

 

Taarifa zilizoifikia SAUTI KUBWA kutoka vyanzo mbalimbali serikalini zinasema kwamba Jenerali Mabeyo ndiye aliomba kikao hicho kifanyike haraka, baada ya gazeti hili kuvujisha habari hizo.

 

Hata hivyo, kauli ya waziri inasemekana kutomridhisha mkuu wa majeshi, ambaye anaamini kuwa kwa kuwa suala hilo limeshavuja, na ni dhahiri kwamba vikosi vingi vya jeshi havifurahishwi na suala hilo, si busara kulifumbia macho, bali rais ashauriwe ili abadili msimamo wake, aruhusu wanyarwanda warudi kwao.

 

Moja ya mambo ambayo yamekera vigogo hao na rais mwenyewe ni jinsi habari hizo zilivyovuja. Si wao tu, maofisa kadhaa wa usalama, hasa wasaidizi wa karibu wa rais, nao wamekuwa wanahaha kuweka sawa suala hili ili “kulinda heshima ya mzee.” Mbali na kikao cha vigogo hao watatu, vimepangwa pia vikosi bya propaganda dhidi ya SAUTI KUBWA, gazeti la mtandaoni ambalo ndilo liliibua sakata hili.

 

Katika njia ya kutapatapa, wapambe wa rais wamepanga kutumia vyombo vyao vya habari kufanya mashambulizi binafsi mfululizo dhidi ya mhariri wa SAUTI KUBWA, wakidhani kwamba mbinu hiyo ndiyo njia ya ama kunyamazisha SAUTI KUBWA na mhariri wake au kumtetea rais – ambaye wao wanadhani “anachafuliwa” kwa habari hizi kuvuja.

 

Mbali na propaganda hizo, wameandaa pia watu wao kushambulia na kuvuruga tovuti ya SAUTI KUBWA zaidi ya mara nne ndani ya wiki moja. Shabaha yao ni kuizuia tovuti hii kuchapisha habari, kwani wanaona zinaibua masuala ambayo vyombo vya Tanzania haviwezi kuandika kwa sababu ya vitisho vya serikali dhidi ya vyombo hivyo, wahariri na wamiliki.

 

SAUTI KUBWA inatambua kuwa kumekuwepo na wanajeshi kutoka Rwanda ambao wanalinda ukuta wa Mererani unaozunguka eneo la machimbo ya madini ya Tanzanite. Kwa mujibu wa makubaliano binafsi kati ya Rais Magufuli na Rais Paul Kagame, kuna vikosi viwili ambavyo vitakuwa vinalinda ukuta huo kwa zamu. Vitakuwa vinapishana kila baada ya miezi mitatu mitatu.

 

Rais Magufuli alizindua ukuta huo mwanzoni mwa mwezi Aprili mwaka huu, lakini hata kabla ya uzinduzi huo walinzi hao wanyarwanda walikuwa wameshaaza kazi kwa wiki kadhaa. Wachambuzi wanasema kuwa sababu yoyote ya kuzuia majeshi yetu kulinda ukuta huo inaibua shaka juu ya uadilifu wa viongozi wanaohusika na usalama kwa upande wa Tanzania.

 

Hatua hiyo ya ukuta huo kulindwa na majeshi ya Rwanda, imekuwa inalalmikiwa chini chini na imeibua minong’ono miongoni mwa vyombo vya ulinzi vya Tanzania.

 

Baadhi ya wanajeshi wameiambia SAUTI KUBWA kwamba hatua hii ni dharau kwa JWTZ, kwani kazi inayofanywa na wanajeshi wa Rwanda pale Mererani si kazi ya kushinda wanajeshi wetu, wala uchimbaji wa madini yale si suala la kimataifa la kuhitaji ulinzi kutoka nje.

Like
34
11 Comments
  1. Mutta L. AB 6 years ago
    Reply

    Hata juzi Alhamis Kuna Mbunge alimhoji waziri mkuu juu ya raia wa kigeni kupewa kazi kwenye maeneo muhimu kama kwenye viwanja vya ndege, bandarini nk japo majibu sikuyaelewa lakini tayari watu wanaonyesha kutoridhishwa na utamaduni wa serikali kuajiri wageni.

    11

    0
  2. Mzalendo 6 years ago
    Reply

    Sauti kubwa endleeni kutupa habari hiz nyeti na muhim kwa Taifa letu ili wahuska wachukue hatua dhid ya upuuzi huu wa kuwapa wanyarwanda rasmali za nchi….

    5

    0
  3. Bobby 6 years ago
    Reply

    All due respect, hizi story tumeziskia kwa zaidi ya miezi mitano . if this was any different from what we heard before ,kwa Uhuru mlionao mngeshaweka details . Msishushe credibility yenu mapema yote hii!

    0

    1
  4. Siji Haji 6 years ago
    Reply

    Endeleeni. Sisi tunautaka mwisho wa mambo haya yote.

    1

    0
  5. NhondoJr 6 years ago
    Reply

    Haya yafanywayo yanasikitisha, bado tuna safari ndefu ya ukombozi wa kiuchumi na kisiasa pia.

    3

    0
  6. mtima nyongo 6 years ago
    Reply

    tunakoelekea sio kuzuri,maana anachokifanya huyu jamaa hata akieleweki kwa watanzania ila kwake na wenzie wanajua wanachokifanya na kuna hatari ya kujiongezea muda wa kutawala

    2

    0
  7. Iman Kyamba 6 years ago
    Reply

    Aisee kuna mengi kumbe hatuyajui haya asante kwa kutujuza. Kazi njema. Kila jambo na wakati wake nalo hili litapita

    4

    0
  8. Emon 6 years ago
    Reply

    We are gone.

    1

    0
  9. Sheri banda 6 years ago
    Reply

    iko siri kubwa kati ya magu na mtutsi,kama si damu zao basi tabia zao.

    2

    0
  10. Albert 6 years ago
    Reply

    Ujumbe kwa CCM kwa kufanikiwa kuhumu nchi kwa kutuwe wageni hadi Ikulu. Tunasubiri uchaguzi ujao mthibitishe kuuzwa kwa nchi.

    0

    0
  11. Joe 6 years ago
    Reply

    Inasikitisha Sana nchi IPO mahali pabaya sana

    0

    0

Leave a Comment

Your email address will not be published.