Mnyika amtaka spika aonyeshe ukali kuhusu maji

Na Mwandishi Wetu

JOHN Mnyika, mbunge wa Kibamba, amemwomba spika wa Bunge awe mkali ili Bunge likwamishe bajeti ya maji na serikali ijipange vema na kuileta upya ikiwa na mashiko. Amesema hoja yake hiyo inatokana na uzoefu kwamba serikali imekuwa inapuuza hoja za wabunge, na kwa miaka yote inawaongopea kwa kutoa ahadi zile zile zisizotekelezeka, huku hali ya upatikanaji wa maji ikiendelea kuwa mbaya mwaka hadi mwaka.

“Mheshimiwa spika, katika suala la sukari ulisimama ukataka kuonyesha ukali. Maji, kwa maisha ya wananchi, ni zaidi ya sukari, kwa sababu ukikosa sukari unaweza ukanywa chai bila sukari. Katika suala la mafuta ulionyesha ukali. Maji ni zaidi ya mafuta kwa sababu ukikosa mafuta unaweza ukapika bila mafuta…

“Mheshimiwa spika onyesha ukali wako katika hili. Na mimi nakuomba sana ukubali kwa sababu tumeshaishauri vya kutosha serikali. Lakini serikali haisikii. Sasa ni wakati wa Bunge kutumia madaraka yake ya kikatiba kusimamia serikali.

“Na mamlaka hayo, Mheshimiwa spika, yanaanza kwa kukubaliana kwamba hii bajeti ya wizara ya maji tusiipitishe sasa. Tukubaliane kwamba bajeti ya wizara ya maji tusiipitishe sasa. Sasa najua kuwa waheshimiwa wabunge wenzangu wana shauku ya kuchangia. Ingekuwa si shauku ya wabunge wenzangu, ningesema nasimama sasa hivi kwa mujibu wa kanuni ya 69 fasili ya kwanza, ambayo inaruhusu mbunge kusimama wakati wowote kutoa hoja ya kwamba mjadala uahirishwe.

“Ningeweza kabisa kusema kwamba mjadala uahirishwe. Sasa ni mwezi Mei, na kuna bajeti zinajadiliwa mpaka mwanzoni mwa Juni, tungesema mjadala uahirishwe mpaka mwishoni mwa Mei, ili serikali, katika makusanyo yake ya mwezi huu…iingize pesa katika wizara ya maji  tuvuke kutoka katika asilimia hii 22 ….tuna uwezo kabisa wa kufaya hivyo kwa kanuni za Bunge…

“Lakini kwa kuwa wabunge wenzangu wana shauku ya kuchangia, bado tunayo nafasi hiyo, mheshimiwa spika, ruhusu wabunge wengine waendelee kuchangia, lakini wakishamaliza wabunge kuchangia kesho, serikali isiruhusiwe kuhitimisha mjadala, mjadala uahirishwe na nipewe nafasi mheshimiwa spika ya kutoa hoja …mjadala uahirishwe mpaka tarehe ngapi…”

Sikiliza kipande cha hotuba hiyo kwa kubonyeza hapa chini:

Like
4
2 Comments
  1. Mtanzania 6 years ago
    Reply

    Hela za maji zimetumika kwa kununulia bombardier, na zingine 1.5 tril.zimepotea.

    0

    0
  2. makaveli 6 years ago
    Reply

    A rubber stamp parliment with a remote controlled speaker of Parliament. Its obvious the super majority will continue to ignore the cries of the citizens of this nation .its a complete waste of time to continue through this path. Let’s face it only a revolution can save us all.

    0

    0

Leave a Comment

Your email address will not be published.