SHAIRI LA MIAKA 60 YA UHURU: MIKAKATI NA UCHUMI, KATIBA KWANZA, UCHUMI BAADAYE

  1. Tangu tupate uhuru, kwa sasa miaka sitini,
    Mipango tunashukuru, imekuwa milaini,
    Kusherehesha uhuru, mjini na vijijini,
    Imetimia sitini, tangu tupate Uhuru.
  2. Mpango miaka mitano, Nyerere aliiweka,
    Mitatu ya mapatano, kuanza kueleweka,
    Kwenye mawasiliano, kilimo kuelimika,
    Imetimia sitini, tangu tupate Uhuru.
  3. Tulianza motomoto, mpaka sitini na nne,
    Tukaona mchakato, katika mambo mengine,
    Wote kwenda mpwitopwiito, kisomo nazo mashine,
    Imetimia sitini, tangu tupate Uhuru.
  4. Kuliwekeza viwanda, mkakati wa viwanda,
    Kote kujengwa viwanda, tukibomoa vibanda,
    Nyerere navyo viwanda, vikashamiri viwanda,
    Imetimia sitini, tangu tupate Uhuru.
  5. Baada ya Muungano, likafata Azimio,
    La Arusha mapambano, Ujamaa azimio,
    Kujitegemea nako, yakawa matazamio,
    Imetimia sitini, tangu tupate Uhuru.
  6. Kuna walioliganga, kuna waloswahibia,
    Kuna waliolipinga, kuhama na kukimbia,
    Wananchi kwa kuganga, wengi hawakukimbia,
    Imetimia sitini, tangu tupate Uhuru.
  7. Huo mwaka wa sabini, hadi sabini na moja,
    TANU iliishabaini, Uhuru mwongo mmoja,
    Mwongozo ulo makini, sote twendwe kwa pamoja,
    Imetimia sitini, tangu tupate Uhuru.
  8. Hali ya umaskini, mapambano si utani,
    Kanisa misikitini, dua hata za ubani,
    Watoto wa mashuleni, wakubwa wa vijijini,
    Imetimia sitini, tangu tupate Uhuru.
  9. Uchumi kutetereka, hadi mwanzo themanini,
    Mwalimu alingátuka, Mwinyi yu madarakani,
    Uliberali funguka, bidhaa zi madukani,
    Imetimia sitini, tangu tupate Uhuru.
  10. Mfumuko wa mabei, mapato yakapotea,
    Sokoni vitu vya bei, uchumi ukapotea,
    Sera kuthibiti bei, zikawa zimekosea,
    Imetimia sitini, tangu tupate Uhuru.
  11. Azimio la Zanziba, mwaka tisini na mbili,
    La Arusha kuliziba, mwaka tisini na mbili,
    Ujamaa liliziba, bila kuwasha kandili,
    Imetimia sitini, tangu tupate Uhuru.
  12. Madeni yalikithiri, nchi ikaelemewa,
    Wakadai kwa kiburi, shuruti tukawekewa,
    Umaskini kiburi, watu wakaelemewa,
    Imetimia sitini, tangu tupate Uhuru.
  13. Akaja wetu Mkapa, na sera utandawazi.
    Dira ya kwake Mkapa, Ukweli pia Uwazi,
    Mali zikabaki kapa, tukauza wawekezi,
    Imetimia sitini, tangu tupate Uhuru.
  14. Madeni kusamehewa, uchumi nao kukua,
    Bei bidhaa kushushwa, ufukara kupungua,
    Ilijipenyeza rushwa, na mali wakachukua,
    Imetimia sitini, tangu tupate Uhuru.
  15. Kikwete alipofika, lake demokrasia,
    Uchumi ukifufuka, rushwa ufisadi pia,
    Umaskini kufuka, makombo tukilambia,
    Imetimia sitini, tangu tupate Uhuru.
  16. Likaja litingatinga, Joni Pombe Magufuli,
    Dola alishalipanga, akisimamia mali,
    Ni yeye tu Tingatinga, kila kitu yake mali,
    Imetimia sitini, tangu tupate Uhuru.
  17. Akiwa yu peke yake, maamuzi yote yake,
    Lawama zikaja kwake, makosa yote ni yake,
    Hata Katiba ni yake, avunje bado ya kwake,
    Imetimia sitini, tangu tupate Uhuru.
  18. Wengi wakilipa kodi, yeye alisha wabinya,
    Samia kupiga hodi, wengi alisha wafinya,
    Apenda walipa kodi, mitaji aipa mwanya,
    Imetimia sitini, tangu tupate Uhuru.
  19. Sera zetu nyingi nzuuri, na sheria zetu nzuri,
    Kinacho gomba shauri, umasikini hatari,
    Tumepambana uzuri, bado mipango mizuri,
    Imetimia sitini, tangu tupate Uhuru.
  20. Bado mipango mizuri, kulinda raslimali,
    Katiba kama ni nzuri, hailindi yetu mali,
    Sasa tuiweke nzuri, ilinde raslimali,
    Imetimia sitini, tangu tupate Uhuru.
  21. Tunautaka usawa, wa kugawana mapato,
    Uchumi ukihodhiwa, ni wote tuwe na pato,
    Uchumi unaoumwa, Katiba ndiyo kokoto,
    Imetimia sitini, tangu tupate Uhuru.
  22. Kikwazo chetu Katiba, isiyolinda uchumi,
    Dawa yake ni Katiba, ili kujenga uchumi,
    Tuandikie Katiba, isiyokuwa UMIMI,
    Imetimia sitini, tangu tupate Uhuru.
  23. Fursa za kiuchumi, kwa wajuku wetu wote,
    Tunaweza kujihami, kwa Katiba yetu wote,
    Uwezi jenga uchumi, kwa Katiba bwetebwete,
    Imetimia sitini, tangu tupate Uhuru.
  24. Kaditama namaliza, shairi li uwanjani,
    Lakini naangaliza, enyi kuweni makini,
    Katiba twaimaliza, mpya ilete nyumbani.
    Hongera miaka sitini, tangu kupata Uhuru.

(Shairi hili limetungwa na Bravious Kahyoza (CEPA; PhD),
1, Desemba 2021)

Like
4