Magufuli anaswa na mtego wa Mobutu

TAYARI kuna jambo moja kubwa ambalo Rais John Magufuli amefanana na Mobutu Seseseko, dikteta wa zamani wa Zaire, ambayo sasa inaitwa Jamhuri ya Kidemokrasi ya Kongo.

Katika utawala wake wa miaka 32 ya ukatili na ubabe, Mobutu alikwapua raslimali za umma, akazielekeza katika kujenga na kuendeleza kijiji cha nyumbani kwake Gbadolite.

Bila ridhaa ya wananchi, alijenga “paradiso” kijijini kwao kwa miradi mikubwa ya maendeleo wakati maeneo mengine yanateketea kwa umaskini.

Alijenga uwanja wa ndege wa kimataifa. Leo uwanja huo umechakaa na kugeuka gofu la popo, panya na wadudu.

Aliweka makao makuu ya wizara ya maji. Jengo hilo chakavu sasa limegeuka madarasa ya shule ya sekondari.

Hoteli kubwa ya kifahari – The Motel Nzekele – imebomoka na kugeuka gofu. Daraja la Gbadolite limebaki nguzo tu.

Jumba lake la kifahari lililohudumiwa na watumishi zaidi ya 700 –  askari 300, wapishi, madereva, na wasaidizi katika majukumu mbalimbali – sasa ni gofu lenye magugu ndani likiwa limezingirwa na vichakaa.

Ikulu ya Gbadolite imebaki gofu la kifisadi, mabaki ya aibu ya utawala wa kidikteta. Mobutu alifanikiwa kutekeleza haya kwa kuwa alijenga utawala wa hofu. Alianza pole pole, kwa kuonyesha sura ya utu, uchapakazi, uungwana na uzalendo – watu wakamwamini, kumbe ndani mwake alikuwa ameficha ufisadi mkubwa.

Rais Magufuli naye ameanza kufuata nyayo za Mobutu. Mbali na miradi mingine mingi anayopeleka nyumbani kwake Chato, anajenga uwanja wa kisasa wa ndege, kwa pesa za walalahoi ambazo hazijapitishwa na bunge kama sheria inavyotaka.

Suala hili liliwahi kulalamikiwa na Tundu Lissu, mbunge wa Singida Mashariki, alipokuwa anazungumzia upendeleo unaofanywa na Rais Magufuli kwa kuteua ndugu na jamaa zake katika nafasi nyeti serikalini, na kupeleka miradi minono nyumbani kwao kibabe.

Liliwahi pia kujadiliwa na Joseph Mbilinyi, mbunge wa Mbeya Mjini, akihoji faida ya kujenga uwanja mkubwa Geita badala ya kuendeleza uwanja wa Mwanza. Akahoji iwapo uwanja huo utakuwa na manufaa yoyote kwa taifa baada ya Rais Magufuli kuondoka madarakani.

Alisema serikali haiwezi kutelekeza uwanja wa ndege wa Musoma alikozaliwa Baba wa taifa Mwalimu Julius Kambarage Nyerere, ikatunza uwanja wa Chato.

Baadhi ya wachambuzi wanasema hotuba hii ilimchoma rais, na kwamba hata kesi na kifungo cha mbunge huyo ni matokeo ya shinikizo kutoka juu kwa sababu ya kuhoji masuala ya Chato, wala si kwa sababu ya maneno yaliyosababisha ashitakiwe.

Majuzi katika kikao cha bunge la bajeti, hoja hiyo imerudiwa na Salome Makamba, mbunge wa viti malumu (Chadema – Shinyanga) kwa msisitizo mpya. Pamoja na mengine, mbunge huyo alisema:

“Tulipitisha hapa (bungeni) shilingi bilioni mbili ikiwa ni pesa ya feasibility study (upembuzi yakinifu) ya uwanja wa ndege wa Chato. Lakini leo tunaongea, bunge hili halikukaa, halikupitisha popote; uwanja wa ndege wa Chato umepelekwa bilioni 42. Na completion stage ya project (hatua ya ukamilifu wa mradi) ya uwanja wa ndege wa Chato ni asilimia 62. Zilipitishwa wapi?…”

Kwa maelezo yoyote yale, huu ni ufisadi mkubwa mno. Chini ya serikali ya Magufuli, shilingi bilioni 40 “zimepigwa.” Kibaya zaidi ni kwamba zimepelekwa Chato, “nyumbani kwake.”

Haya yanatokea wakati wananchi bado wanahoji zilikopelekwa trilioni 1.5 ambazo mdhibiti na mkaguzi wa hesabu za serikali (CAG) amesema hazijulikani zilipo.

Kuna taarifa za kuaminika kuwa fedha hizi “zimechotwa” na kuwekwa kwenye akaunti maalumu ambayo inasimamiwa na rais na “mtu wake” mmoja katika wizara ya fedha. Shabaha ya akaunti hiyo ni kufadhili Chama Cha Mapinduzi (CCM) katika uchaguzi mkuu ujao, kwani Rais Magufuli ana hofu ya kuomba fedha za wafanyabiashara ambao, hata hivyo, wanalia ukata kwa sababu serikali yake imewafilisi.

Ufisadi huu unamomonyoa sifa ambazo Rais Magufuli amekuwa anajipa kwamba yeye ni mtu safi anayepigana na ufisadi. Zinaweza kushangaza wasiojua utendaji wake. Lakini kwa wanaomjua, wala hawatarajii rais ashtuke kwa ufisadi huu.

Wanamhusisha moja kwa moja kwa kuwa wanafahamu jinsi alivyo mpenda sifa. Kama asingehusika angekuwa mwepesi kuchukua hatua dhidi ya waliokwepesha fedha hizo. Lakini kwa kuwa amekaa kimya na fedha zimeendelea kutumika bila idhini ya bunge, ni wazi ameridhia na ameshiriki “wizi” huo.

Hoja hii inakaziwa na kile alichosema Zitto Kabwe, mbunge wa Kigoma Mjini, kwamba imekuwa tabia ya Magufuli “kupoteza” fedha za umma tangu alipokuwa waziri.

Zitto anasema: “…mimi nimekuwa Mwenyekiti wa PAC/POAC (kamati ya bunge ya ukaguzi wa hesabu za serikali kuu na mashirika ya serikali) kwa miaka minane (8), ninajua kusoma, kuchambua na kutafsiri Taarifa ya CAG. TZS 1.5trn hazina maelezo, hazipo Benki Kuu na Maelezo ya Naibu Waziri Fedha leo ni kujikosha tu.

“Nikiwa Mwenyekiti wa PAC, Mwaka 2013 Waziri wa Ujenzi John Pombe Magufuli alikutwa na Hoja ya ukaguzi ya TZS 252 bilioni ya ujenzi wa barabara hewa ambayo mpaka sasa haijajibiwa na utaikuta kwenye Hoja za CAG za mwaka 2016/17. Hivyo ni Kawaida yake kutoheshimu sheria za Fedha na kutojibu Hoja za Ukaguzi.”

Magufuli ametumbukia kwenye ufisadi mapema mno kuliko watangulizi wake, na ndani ya miaka miwili amehusishwa na ufisadi mkubwa ambao haujawahi kutokea.

Ndiyo sababu hataki vyombo vya habari huru. Ndiyo maana anaogopa mikutano ya hadhara ya vyama vya upinzani. Ndiyo maana anadhibiti bunge kwa kumtumia spika na naibu spika.

Aweza kufunika uso wake kwa viganja kama nyani, halafu kwa akadhani wananchi hawaoni na hawajui. Tayari wanajua.

Like
61
21 Comments
  1. Eliatosha 6 years ago
    Reply

    Nimekusoma mkuu

    0

    0
  2. Solokondo 6 years ago
    Reply

    Afadhali Mkuu Ngurumo humu ndio tunapata vitu vya uhakika

    0

    0
  3. usoni kamawatu 6 years ago
    Reply

    Magufuli ni mtu hatari sana kwa taifa letu la Tanzania

    0

    0
  4. Msomaji 6 years ago
    Reply

    Ahsante kwa makala nzuri… Tafadhali tunaomba ujiunge na Instagram ili kuwafikia wengi na kupromote website yako.

    0

    0
    • Ansbert Ngurumo 6 years ago
      Reply

      Tayari. Asante kwa ushauri.

      0

      0
  5. Jinyam 6 years ago
    Reply

    Shortly as a citizen, am so sad with African leaders. Actually this is how they do for their benefits not country.

    0

    0
  6. The Boss 6 years ago
    Reply

    Makala nzuri… Yani endelea kufichua uozo wa serikali hii. Labda Watanzania wata amka, kujua nini kinachoendelea. Magufuli ni raisi na muda wake utapita tu, atakuja mwingi. Hakuna atakae ishi milele. Kila mtu anatakiwa ajue kuna kufa pia. Ukifa historia yako imefungwa. Ahsante sana kwa hii makala nzuri sana. Mungu akuongoze.

    0

    0
  7. Dodo 6 years ago
    Reply

    Jamani, Mungu atunusuru na hawa viongozi wachumia tumbo.

    0

    0
  8. Popcorn 6 years ago
    Reply

    Good

    0

    0
  9. mtumwa 6 years ago
    Reply

    Duuuuu⌚ mda haurudi nyuma Mobutu kaacha kilakitu kaenda

    0

    0
  10. mtima nyongo 6 years ago
    Reply

    dalili za kuwa kama mobutu zimeshaonekana na si ajabu akamzidi,

    0

    0
  11. Mtanzania 6 years ago
    Reply

    Nimekupata mkuu! Tanzania Revolution

    0

    0
  12. Mtanzania 6 years ago
    Reply

    Nimekupata mkuu sana uko right! Tanzania Revolution

    0

    0
  13. Isihaka athman 6 years ago
    Reply

    Unajitahidi sana kumchafua lakini ungetafuta vitu vingine acha propaganda nyepesi , unafeli sikubaliani na wewe kama ambavyo wengine wamekubaliana na wewe

    0

    0
    • Ansbert Ngurumo 6 years ago
      Reply

      Simchafui wala simsafishi. Sina uwezo huo. Amejichafua mwenyewe. Mimi nimeona na nimesema; na ndiyo kazi yangu.

      Sana sana waweza kudhani najichafua mwenyewe kwa kushika uchafu huu. Lakini nitafanyaje? Ndiyo kanuni ya kufanya usafi. Nasafisha nyumba!

      Unalaumu mfagio, aliyeshika mfagio, au aliyeleta uchafu?

      2

      0
    • Molimoli 6 years ago
      Reply

      Ni mwenye akili ndogo kama ya Nyumbu ndiye anaweza kumtetea Magufuli

      0

      0
  14. Mtanzania 6 years ago
    Reply

    Huyu ni Mabutu style. Arising new african dictator!!CCM inajifanya haioni?

    0

    0
  15. Mayala 6 years ago
    Reply

    Jiunge na Instagram au ufungue App ili tuweze kupata habari kwa urahisi zaidi

    0

    0
  16. Makina 6 years ago
    Reply

    Mr Ngurumo, Mm ni mmoja Wawafuatiliaji wa makala yako baada ya toleo lako kwenye Gazeti la Mwananchi kuhusu ” Barua ya wazi Kwa Raisi Magufuli”… Kwa kweli Mungu amekujalia kipaji cha kuandika na ukaeleweka…. Kaka mm niombe kujua jambo kwani mm naamini wewe ni mtetea haki za binadamu na hufungamani au husukumwi na hisia zisio za kinadamu. Kwakusema haya, Na pia nikijua kabisa wewe umebobea kwenye utafiti wa habari zetu Tanzania, Je nikweli serekali ya Tanzania imekuwa na ilikuwa ina wadhulumu waislamu kwenye nyanda zote? Elimu na Biashara? Asante

    0

    0
  17. Ngoswe 6 years ago
    Reply

    ????kazi nzuri kaka

    0

    0
  18. makaveli 6 years ago
    Reply

    RESISITANCE RESISITANCE RESTINCE .REVOLUTION REVOLUTION REVOLUTION .We must all sing this song the rest is just a distraction.

    0

    0

Leave a Comment

Your email address will not be published.